Wasanii waiangukia Serikali kuingilia kati soko la filamu

 


Mkuu wa Wilaya ya Geita, Wilson Shimo akizindua Filamu ya KOSA LA MAMA kama sehemu ya kuunga mkono juhudi za kuendeleza tasnia ya uigizaji nchini.

Na Yohana Paul, Geita

WASANII wa Filamu mkoani Geita wameiomba Serikali kuendelea kuwaunga mkono na kuwawekea mazingira rafiki ya kuendeleza sanaa ikiwemo kuweka usimamizi madhubuti wa soko la filamu ambalo lina changamoto kubwa kwa sasa ili kuifanya tasnia ya uigizaji kutengeneza ajira kwa vijana.

Akizungumza kwa niaba ya wenzake wakati wa uzinduzi filamu yake ya KOSA LA MAMA, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Maigizo ya Kapaya The Great, Michael Kapaya amesema serikali ikiweka usimamizi na kanuni thabiti kwenye soko la filamu.

Amesema kw akufanya hivyo wataweza kujikwamu kiuchumi ambapo pia ameishauri Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, kuandaa matamasha ya filamu yatakayowasaidia wasanii kutangaza kazi zao.

Aidha, Kapaya ameviomba vyombo vya habari kuipa nafasi sanaa ya uigizaji kama ilivyo kwa uimbaji kwani sanaa hiyo haiwezi kukua kama hakuna ushirikiano wa vyombo vya habari na kudokeza kuwa maudhui ya filamu yake ya KOSA LA MAMA yanalenga kuigusa na kuielimisha  jamii juu ya wajibu wa mama kipindi cha malezi kwa mtoto mchanga.

Mkuu wa Wilaya ya Geita, Wilson Shimo amesema malengo na maono yaliyomo ndani ya filamu ya KOSA LA MAMA yanatoa taswira ya  namna gani vijana ambao wanaibukia kwenye fani tofauti wanahitaji msaada na kuungwa mkono ili waendelee kuelimisha, kuburudisha na kujipatia kipato.

Amesema ofisi yake ipo tayari kuwashika mkono wasanii wote hususani wale walioonyesha nia, na wataendelea kuwaelekeza vijana juu ya hatua za kupitia kupata mikopo kutoka asilimia 10 inayotengwa kwa ajili ya mikopo kwa makundi ya vijana, kina mama na watu wenye ulemavu ili waweze kujiendeleza kufikia malengo yao.

Shimo alisema kutokana na uwepo wa tasnia nyingi na kazi za sanaa wanatarajia kuwekeza kukuza tasnia ya filamu wilayani Geita na watahakikisha kila mwaka wanasaidia tasnia nyingine ili kupanua uwigo wa fursa za ajira kwani Filamu ya KOSA LA MAMA imetoa mwanga kwa kutoa ajira za muda mfupi kwa takribani vijana 40 ambayo ni matunda ya sanaa.

Naye mdau wa maendeleo na sanaa mkoani Geita, Daniel Haji amesema filamu ya CHOZI la MAMA imewafundisha uhitaji wa wadau wote mkoani GEITA kushikamana kukuza sanaa hiyo na hata kuutangaza utamaduni wa mkoa na taifa kupitia tasnia ya filamu ambazo mbali na kuburudisha na kuelimisha pia ni sehemu ya ajira.

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu watoa tahadhari ya chanjo kwa wajawazito, wagonjwa